Menu

About Publisher
Ukurasa Wa Mbele
Nyakati Duniani
Habari Mbalimbali
Barua za Wasomaji
Kauli Ya Mhariri
Makala 
Mjadala
Matangazo 
Bible Study
Tuwasiliane 
GuestBook Page

WWW.NYAKATI.FAITHWEB.COM


MHINDI AJIITA MUNGU MWENYE NGUVU

Na Masha Otieno Nguru, JR MAY 4 - 10
KATIKA hali inayoonyesha dhahiri kwamba kauli ya Bwana Yesu mwenyewe kuwa katika siku za mwisho wataibuka watu wakijiita miungu na makristo sasa inathibitika, mtu mmoja ameibuka na kuanzisha himaya yake ya kidini na kujiita mungu. Mtu huyo anayejiita mungu mwenye nguvu, anazungukwa katika himaya yake hiyo na anaowaita wenye uhai wanne huku akitolewa sadaka zinazomtajirisha sana na kumfanya awe bilionea.

Sambamba na matukio hayo, mwanadamu huyo anadai kwamba ana uwezo na maamuzi ya kufufua wafu na kuponya kimiujiza. Tena anasema kwamba ana mamlaka ya kuwakutanisha waumini wa dini fulani na yule wanayemwamini akitolea mfano kwamba anaweza kuwakutanisha Wakristo na Bwana Yesu sambamba na Waislamu na Muhammad.

Kwa mujibu wa gazeti la Indias Today, la mwezi uliopita, Mungu mtu huyo maarufu kwa jina la V. Vijaykumar (53), anakaa kwenye kiti cha kifahari ndani ya jumba moja la fahari kubwa na huvalia kanzu ya bei aghali yenye mchanganyiko wa rangi ya bluu na nyeupe huku kichwani mwake akivaa taji inayoelezwa kuwa nayo ni ya bei ya juu sana.

Habari zinaeleza kwamba mungu mtu huyo anapatikana katika kitongoji cha Nemam Ashram, huko Tamil Nadu, katika wilaya ya Thiruvallur nchini India.

Gazeti hilo linahabarisha kuwa Vijaykumar, ana wafuasi wapatao milioni moja duniani kote chini ya dini au mtandao wao uitwao Kalki. Linasema kwamba Vijaykumar pia anajigamba kwamba yeye ni mtabiri na kwamba anatabiri kuwa kati ya mwaka 2005 na 2025, dini nyingine zote zitafutika huku ikibaki ya kwake.

Inaelezwa kwamba kwa sasa anawatoza watu Ruupia za India kati ya 500 na 2500 kwa ajili ya kujifunza masomo ya imani yake kwa muda wa kati ya siku tatu na juma moja. Vijaykumar anajiita "Supermarket" akimaanisha kwamba ana uwezo wa kutoa kila kitu na baraka mbalimbali na kuziunganisha dini na mitume wao.

Gazeti hilo linaongeza kwamba Vijaykumar anaendelea kutajirika sana kila siku kwa kupokea sadaka na michango ya waumini wake wanaoamini kwamba wanaweza kubarikiwa na yeye na kutabiriwa mambo yao mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwatabiria wachumba wanaowataka na kama wanahitaji utajiri. Hata hivyo watu kadhaa nchini humo wameendelea kumpinga na wengine kumshitaki mahakamani kwa utapeli huku wengine wakihoji uhalali wa kujiita mungu ilhali ana mke na watoto wa kimwili wa kiume na wa kike.

Inaelezwa kwamba wengi wanapinga imani yake ambayo inasisitiza kuwa katika siku za usoni, dunia itakuwa mahali bora pa kuishi baada ya kutwaliwa na utawala wa Kilki chini ya usimamizi wake. Kwenye kitabu cha Mathayo 24:4-5, Yesu alipokuwa akizungumza na wanafunzi wake katika mlima wa mizeituni, aliwaonya akisema: "Angalieni, mtu asiwadanyanye kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema mimi ni Kristo nao watadanganya wengi."

Mmoja wa watu waliodanganywa ni Bw Sujay Krishna (25), ambaye aliamua kuacha kozi yake ya Uhandisi katika Chuo Kikuu kimoja kule India na kuungana na Vijaykumar. "Niliona mpira mdogo wa dhahabu ukitoka kwa Vijay kumar na kuja kutoboa kichwa changu na kuingia kwangu. Tangu hapo niliacha mafunzo ya uhandisi na kujiunga na Kalki.

Imani hiyo ilianzishwa mwaka 1989 baada ya mungu mtu huyo kuacha kazi yake ya ukarani katika moja ya mashirika ya Bima nchini India ambapo sasa si karani tena ni bilionea, mungu mtu huku akizungukwa na wenye uhai wanne, wawili kulia na wawili kushoto wakisubiri kutatua shida yoyote inayoweza kumtokea Vijaykumar.

WANYAMA WAREJEA ISRAEL KUTIMIZA UNABII

CW News, Feb 16 - 22
BAADHI ya wataalamu wa Biblia wamesema kwa jinsi ya ajabu wanyama mbali mbali waliokuwa na maana kubwa kinabii ambao walishatoweka katika ardhi ya nchi takatifu ya Israeli nao wamerejea tena, jambo ambalo linaonyesha kutimia unabii wa Biblia, baada ya Mungu kuwarejesha tena kwao (Israeli) Wayahudi.

"Jambo ambalo ni wachache wanaolijua, ni kwamba wanyama waliotajwa katika Biblia ambao kwa karne nyingi walikuwa wametoweka nao wamekuwa wakirejea," amesema Mwandishi Chris Mitchell, wa Shirika la habari la CW News.

Amesema kuwa mwaka 1969 Mamlaka ya Utunzaji wa Maliasili ya Israeli, ilianza kuwaandalia wanyama hao mazingira ya kuwafaa kuishi, hususan katika maeneo yale waliyowahi kuishi hapo kale, jambo ambalo limeonyesha mafanikio makubwa.

Mamlaka hiyo imeandaa miradi mikuu miwili ijulinayo kama 'Hai bar'. Wa kwanza uko kwenye Mlima wa Karmeli, katika mkoa wa Haifa, mahali ambako Nabii Eliya alishindana na miungu ya kipagani na wa pili katika eneo la Bonde la Arava karibu na Eilat. Miradi hii yote miwili ina kazi maalum ya kutetea na kulinda haki za wanyama ambao waliishi katika maeneo hayo kulingana na kumbukumbu za Biblia.

Avinoam Luria, ni Mkurugenzi wa Hai Bar katika mlima wa Karmeli. Anasema, " Hai Bar kwa kweli ni ukanda wa Kibiblia wa wanyama ambao walikuwa wametoweka nchini katika miaka 200 iliyopita."

Mamlaka ya Maliasili ya Israeli imesema inaona suala hilo kama Biblia kuishi kidhahiri kabisa miongoni mwao.

Luria alisema, "Hii inaweza kuwa kutimia kwa unabii, kwa kuwa wanyama hawa nao hii ni nchi yao. Na haki yao ya kurejea hapa, naweza kusema ni sawa tu na ile tuliyo nayo sisi na sio pungufu ya hapo."

Wanyama watajwao katika Biblia wanaokadiriwa kufikia 350 wamesharejea Israeli.

Mingoni mwa viumbe vinavyorejeshwa Israeli ni ndege aina ya Tai, ambao hufananishwa na manabii wa Mungu kutokana na sifa yao ya kuona mbali kuliko viumbe wengine wote.

Uri Beidats anayefanya kazi kama Mkurugenzi wa Israel Nature & Parks Authority aanasema, " (Mnyama aina ya) Ayala ni alama ya kabila la Naftali. Simba alikuwa alama ya kabila la Yuda, na nyoka alikuwa alama ya kabisa la la Dani, wakati mbwa-mwitu alikuwa alama ya kabila ya Benyamini na kadhalika."

Baada ya kupoteza utaifa wao kwa karibu miaka 3000 iliyopita, Wayahudi walianza kurejea Mashariki ya Kati (Israeli) zaidi ya miaka 50 iliyopita ambapo mwaka 1948 Umoja wa Mataifa uliwatangazia taifa lao huru, na tangu wakati huo wamekuwa wakiendelea kurejea, kama ilivyotabiriwa katika Biblia.

Wakati wa Yesu Wayahudi walikuwa chini ya ukoloni wa Warumi ambapo baadaye walisambaratishwa na adui zao na kutapakaa tena duniani kote, lakini jambo la ajabu ni kwamba katika kipindi chote cha miaka 3000 ya kupoteza utaifa wao bado wamehifadhi lugha yao na mila zao.

VIONGOZI WA KANISA WATUPWA JELA KWA KUHUBIRI INJILI

CBN, Vietnam, APRIL 20 - 26
KATIKA mfululizo wa mateso dhidi ya Wakristo duniani, viongozi wawili wa kanisa nao wamekamatwa na kupelekwa gerezani kwa kile wanachotuhumiwa kuwa ni kuendesha huduma ya injili kinyume cha sheria za kikomonisti za hapa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa juzi na Shirika la Kimishenari la Christian Aid Mission (CAM), viongozi wawili wa kanisa liitwalo Nong-ing Church Service, Bw. Ton (58) na Bw. Serun (45), walikamatwa Aprili tatu, mwaka huu na kupelekwa moja kwa moja gerezani baada ya kukutwa wakiendesha mkutano wa injili nje ya kanisa lao.

Pamoja na kukamatwa kwa viongozi hao, pia serikali iliagiza kufungwa kwa huduma ya injili ya kanisa hilo moja kwa moja sambamba na kupiga marufuku kusanyiko la aina yoyote.

Baadhi ya watu walioshuhudia tukio hilo, waliliambia shirika la CAM kuwa kanisa hilo limekuwa shabaha ya serikali kutokana na kutembelewa na viongozi wa ngazi za juu wa serikali ya Marekani hivi karibuni.

Aidha imeelezwa kuwa wamarekani waliotembelea kanisa hilo waliwakuta waumini wakiwa wamevaa nguo nyeusi kuonyesha kuwa wako kwenye mateso makubwa kutokana na kuwa wahanga wa msimamo mkali wa kidini wa serikali ya kikomonisti ya nchi hiyo.

Taarifa hiyo imesema kuwa serikali hiyo ya kikomonisti baada ya kufunga kanisa, imenyakua kwa mabavu jengo lililokuwa likitumika kama nyumba ya ibada na kuligeuza kuwa moja ya ofisi zake.

Katika tukio lingine linalofanana na hilo, kanisa moja lililopo katika wilaya ya Chonburi, limefungwa na serikali na waumini wake kupigwa marufuku hata kuabudu nje ya kanisa lao walilojenga wenyewe wala kuendesha aina yoyote ya maombi.

Kanisa lingine lililofungwa katika kampeni hiyo ya kufutilia mbali huduma ya Injili huko Vietinam, ni lile la Ethnic Bru, lililoko mpakani mwa Vietinam ambapo kiongozi wake Bw. Koy, pamoja na familia 13 za waumini wa kanisa hilo, wamefukuzwa kutoka majumbani mwao na sasa wanaishi kwa kutanga tanga.

Shirika la CAM limewataka wakristo kote ulimwenguni, kupiga magoti na kumuomba mungu awaokoe watu hao walioko matesoni.

Aliyempokea Yesu akatwa vipande vinne

Mwandishi wetu na Mashirika ya Habari, Agosti 10 - 16
MTU mmoja ambaye alikuwa Muislamu kwa muda mrefu kabla ya kumpokea Bwana Yesu na kuwa Mkristo, ameuawa kinyama na Waislamu wenye imani kali wakitumia kigezo cha sheria za kiislamu (Sharia) ambazo zinatoa ruhusa kwa Mwislamu kumwua Mwislamu mwenzake ambaye anabadili dini kuwa Mkristo.

Kwa mujibu wa shirika la Barnabas Fund linalojishughulisha na utoaji wa misaada kwa Wakristo walioko kwenye mateso, mtu huyu aliyetajwa kwa jina la Arafat Ahamed, ambaye ni mkazi wa eneo la Gaza linaloongozwa na utawala wa ndani wa Palestina, alikumbana na mauti hayo mwanzoni mwa wiki iliyopita.

Barnabas Fund, likikaririwa na mtandao uitwa "World Net Daily.com" linasema kuwa Bw. Ahamed aliondoka nyumbani kwake siku kumi zilizopita akiagana vyema na familia yake kuwa anakwenda kutembelea eneo la milimani ambalo pia linaongozwa na utawala wa ndani wa Palestina akibeba Biblia pamoja na mkanda wa Video lakini hakurejea nyumbani.

Shirika hilo linasema kuwa siku kumi baada ya Bw. Ahamed kuondoka nyumbani, mwili wake ulirejeshwa na watu ambao hawakufahamika vyema na kuwekwa nje ya nyumba yake huku ukiwa umegawanywa vipande vinne na wakaonywa kuwa mwingine yeyote atakayeusaliti Uislamu basi atakabiliwa na adhabu kama hiyo.

Hata hivyo Barnabas Fund linasema kuwa haliwezi kutoa habari zote zinazohusu mauaji hayo kutokana na ukweli kuwa familia na marafiki wa Bw. Ahamed bado wako katika hatari kubwa ya kuuawa na Waislamu wenye imani kali.

Shirika hilo lenye kutetea Wakristo wanaoteseka karibu ulimwenguni kote linasema kuwa hali ni mbaya zaidi katika ardhi takatifu ya Israeli kwa kuwa kikundi cha kigaidi cha Hamas kina fungu la fedha toka nchi moja ya kiarabu (Jina tunalihifadhi) kwa ajili ya kuua Wakristo waliookoka wakiutupilia mbali Uislamu.



Kwa Mujubu wa Sharia, mtu yeyote ambaye atabadili dini kutoka Uislamu na kuwa Mkristo adhabu yake ni kunyongwa.

Copyright © 2002-2003 Nyakati.


Vichwa vya Habari

Hamadi waapa kuwaandama Wayahudi na wakristo Duniani pote

Wanyama warejea Israeli kutimiza unabii

Viongozi wa Kanisa watupwa jela Kwa kuhubiri Injili

Israeli yaionya Syria kwa kuipa Kadi Nyekundu